JB afanya kazi na rachie watengana?


JB.jpgSIMULIZI inazidi kunoga. JB anaendelea kueleza kila kitu alichopitia maishani mwake, sasa yuko katika kipengele cha safari yake ya sanaa. Tangu wakati wa maigizo hadi sasa kwenye filamu, ambako anaendelea kutengeneza pesa kupitia kazi hiyo ya uigizaji.
Wiki iliyopita, alieleza jinsi alivyoanzisha kampuni ya kuzalisha filamu ya Jerusalem. Akieleza pia ugumu aliokutana nao. Je, nini kilifuata?
TWENDE PAMOJA…

“Kwa hiyo nikabaki peke yangu kwenye kampuni, sikukata tamaa, nikajipa moyo na kuendelea kukaza buti,” anasema JB kwa msisitizo zaidi.
“Unajua filamu ya Kanisa la Leo, ilichelewa sana kuingia sokoni, kwa hiyo nikawa nimetengeneza filamu ya Agano la Urithi, ambayo iliingia sokoni kabla ya ile ya mwanzo,” anasema.
“Wakati naendelea kuwaza, nikaamua nimuite Richie ili tuwe pamoja kwenye kampuni yangu, nikaanza kumshawishi, nikamshawishi aachane na kazi yake kwenye kiwanda cha Chai Bora, kwa kuwa Richie anapenda sana kuigiza, aliamua kuacha kazi na kuja kuungana na mimi kwenye kampuni yangu ya Jerusalem,” anabainisha JB.
“Nikamfanya kuwa partner, yaani tukagawana hisa kwenye hiyo kampuni, tukatengeneza filamu ya Stranger, filamu ambayo hakika sitaisahau katika maisha yangu ya uigizaji,” anasema JB huku akijirekebisha vyema kwenye kiti.
“Kwa nini kaka,” najikuta nikimtupia swali huku nami nikiirekebisha vyema tai yangu.
“Ilikuwa ni filamu ya kwanza kunipa tuzo kama Muigizaji Bora wa Kiume, hakika sinema hiyo ilinipa morali na bidii zaidi katika kufanya kazi yangu ya uigizaji,” anasema JB na kunitazama usoni kwa muda kabla hajaendelea.
“Basi, heshima ikaanza kujengeka tena, lakini kwa wakati huo, mtu aliyekuwa akiheshimika zaidi kwenye tasnia ya filamu ni Gabriel Mtitu wa Game First Quality Tz Limited, akiwa na wasanii wakubwa kama Ray na Kanumba, hakika alikuwa ameliteka sana soko,” anasema.
“Ngoja niwe mkweli katika hili pia, huwezi kutaja orodha ya watu waliochangia kuinua sanaa ya uigizaji nchini, usimtaje Mtitu wa Game, huwezi, wapo wengi kama Sultan Tamba, Musa Banzi, hawa ni watu ambao wana mchango mkubwa sana kwenye ukuaji na upanukaji wa sanaa ya uigizaji hapa nchini,” anasema JB bila kupumzika.
“Kwa hiyo, ushindani ulikuwepo mkubwa, lakini pamoja na hayo, mimi na Richie tuliendelea kujipa moyo kuwa, lazima tufike mbali kwa kazi hii ya sanaa,” anasema.
Kwa wakati huo, tulikuwa tukisambaza sinema zetu na Kampuni ya Mwananchi Store, chini ya msambazaji Farhaji Mohamed,” anasema JB.
“Kwa hiyo, kazi zikaendelea kufanyika, tukaigiza sinema moja ya Swahiba, ambayo kwa hakika kabisa ilitupa jina kubwa sana kwenye tasnia ya filamu hapa nchini, ni filamu ambayo iliongeza heshima kwenye kampuni yetu,” anasema JB.
“Kuna kitu nataka kusahau, unajua watu wengi hudhani nimeanza kuigiza na Mzee Majuto  kwenye filamu za Shikamoo Mzee na Nakwenda kwa Mwanangu, la hasha, mzee huyu niliwahi kuigiza naye sinema moja huko nyuma, lakini haikujulikana sana, iliitwa Pwaguzi,” anasema JB na kusindikiza maelezo hayo kwa kicheko cha juu.
“Pia, filamu ya Swahiba, ndiyo iliyomtambulisha kwenye ramani ya uigizaji msanii mmoja mkali sana wa kike hapa Bongo, si mwingine bali ni Rose Ndauka, tulikutana naye huko kwao maeneo ya Kigogo, tukaamini anaweza kuigiza, tukampa mafunzo na kuigiza naye sinema hiyo,” anasema.
“Hata hivyo, mwishoni mwa mwaka 2007 kama sikosei, Richie aliniambia, kutokana na ukuaji wa sanaa kwa wakati huo, ni bora naye ajitegemee kwa kuanzisha kampuni yake ya kuzalisha filamu, niliumia sana, maana nilikuwa nimemzoea sana Richie, lakini sikuwa na jinsi,” anasema.
“Richie akaanzisha Kampuni ya Bulls, ambayo filamu ya kwanza kuigiza iliitwa Mahabuba, alinishirikisha pia, tulifanya kwa moyo wote kabisa na maisha yakaendelea,” anasema.
“Nikaendelea na kuzalisha filamu, nikaamua kuungana tena na msanii nguli ambaye kwa sasa ni marehemu, Adam Kuambiana, ambapo nilimuajiri kama muongozaji wa filamu za kampuni yangu,” anasema JB.
Je, nini kitafuata? Usikose wiki ijayo
Newer Posts Older Posts

© Copyright Chiriku Mzee

Designed By Chiriku Mzee

Blogger Templates

Back To Top