Mke kumgeuza mumewe zezeta kishirikina


Siku zote najua kila mtu anapenda kuwa na mtu ampendaye. Najua fika hata wewe unayesoma hapa unatamani mpenzi wako akupende kama unavyompenda wewe ikiwezekana yeye azidishe mapenzi.
Hicho si kitu kibaya kwani najua raha ya kupendwa. Lakini sasa wakati hali ikiwa hivyo huwa nawashangaa sana wale wanawake ambao wanafikia hatua ya kutumia pesa zao nyingi kwenda kwa waganga eti ili waume au wapenzi wao wawapende, wawanyenyekee, hivi huu ni uungwana kweli?
Yaani mwanamke na akili zake, anadunduliza pesa kisha badala ya kuzifanyia mambo ya msingi anakwenda kwa sangoma eti ili akamzubaishe mume asifikirie wanawake wengine zaidi yake, ni uungwana?
Mimi sikatai kwamba kila mmoja lazima afanye awezalo kuhakikisha anamshika vilivyo mtu wake lakini sidhani kwamba kumuendea mumeo kwa mganga ni jambo la busara.
Mbaya zaidi wengine huenda huko kisha kuomba wapewe dawa za kuwapumbuza waume zao, eti kila anachotaka apewe, akisema lolote asikilizwe, akimwambia mume leo hakuna kwenda kazini, mume akubali, aah kweli umgeuze mumeo awe zezeta kiasi hicho! Maisha gani hayo?
Kama umeshindwa kutumia njia sahihi za kumshika huyo mume wako heri umuache akatafute mwingine na wewe uchukue hamsini zako lakini siyo kwenda kununua limbwata la kulazimisha mambo yasiyoleta picha nzuri kwenye jamii.
Wakati mwingine inasikitisha sana, unakuta mwanaume kwenye familia yake hana sauti kabisa, kila kitu anachosema mke yeye hewala. Mke akitaka kwenda kwenye mambo yake, hata asipoaga, asiulizwe na kweli mume ananyamaza.
 Mume akipokea mshahara wake, moja kwa moja kwa mkewe, eti mke ndiye anaupangia bajeti huku akijisevia za kwake za kufanyia mambo yake.
Ndugu au wazazi wa mume wakihitaji msaada wa fedha, mke huzuia wasipewe na mwanaume husika hukubali kwa kuhofia kumpinga mkewe atakuwa kamkosea sana.
Mwanamke kumfanyia hivyo mumewe hakuna ubaya, ambapo huwajali wazazi na ndugu zake ambao wakiomba msaada wowote hutekelezewa ‘fasta.’
Mume anapangiwa ratiba ya kufanya kazi za ndani, hee jamani! Hayo ndiyo mahaba kweli au kudhalilishana?
 Hivi mumeo akiwa zezeta wewe unasikia raha gani? Kwamba wewe sasa uwe ndiye mwenye sauti, ukisema mume ananywea! Noh! Hii siyo sawa na wanawake mnaifanya hivyo mnakosea na siyo uungwana
Newer Posts Older Posts

© Copyright Chiriku Mzee

Designed By Chiriku Mzee

Blogger Templates

Back To Top